Tuesday, May 27, 2014

WAMACHINGA WAMUUA ASKARI JIJINI DAR ES SALAAM


Marehemu Stephano Benjamin Komba (36) ambaye aliyekuwa na cheo cha sajenti.
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida vijana wanaodaiwa ni Wamachinga wamemuua askari mmoja wa Jiji la Dar es Salaam kwa kumpiga na stuli kichwani wakati akitimiza majukumu yake.



Akizungumza na waandishi wetu mwishoni mwa wiki iliyopita Hospitali ya Taifa Muhimbili wakati wa kuuaga mwili huo, Mkuu wa Oparesheni Manispaa ya Ilala, Charles Wambura alimtaja marehemu kwa jina la Stephano Benjamin Komba (36) aliyekuwa na cheo cha sajenti.



Mke wa marehemu Stephano Benjamin Komba (mwenye kilemba cheupe).

Alisema tukio hilo lilijiri Mei 16, mwaka huu, saa 7.30 mchana kwenye Mtaa wa Raha Kariakoo.
“Marehemu alikuwa na askari wengine walikamata baadhi ya bidhaa za Wamachinga kwa lengo la kuwaondoa lakini ghafla walivamiwa na kundi la wafanyabiashara hao ambapo Sajenti Komba akapigwa kichwani kwa stuli hali iliyomfanya apoteze fahamu kwa kuvuja damu nyingi.

“Askari walipambana na hao Wamachinga na kufanikiwa kumuokoa Sajenti Komba lakini akiwa na hali mbaya.

Mke wa Marehemu Stephano Benjamin (katikati) akisaidiwa na jamaa wa karibu msibani kumuaga marehemu mume wake.

“Walimkimbiza Kituo cha Afya cha Mnazi Mmoja lakini hali yake ilizidi kuwa mbaya ndipo walimpeleka Muhimbili ambapo alifariki dunia saa 2:00 usiku,” alisema Wambura.
Mwili wa marehemu uliagwa Ijumaa iliyopita nyumbani kwake Mbagala na kusafirishwa kwao Songea, mkoani Ruvuma kwa mazishi.

Wambura aliongeza kuwa, hakufurahishwa na kitendo hicho cha Wamachinga kuchukua sheria mkononi.Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Ilala, SACP Marietha Minangi alikiri kutokea kwa tukio hilo na kuwataka wananchi kutii sheria bila shuruti.

No comments:

Post a Comment