Wednesday, March 26, 2014

MPASUKO MKUBWA BUNGE LA KATIBA

Wakati kamati 12 za Bunge Maalumu la Katiba za kupitia Rasimu ya Katiba zikitarajiwa kujulikana leo, hali ya mpasuko katika Bunge hilo imezidi kuwa dhahiri ikichochewa zaidi na hotuba ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa Ijumaa iliyopita.Mpasuko huo unajidhihirisha dhahiri baada ya sasa kuibuka makundi kinzani ndani ya Bunge Maalum la Katiba.Wakati kundi la wabunge wanalounda Umoja wa Kutetea Katiba ya Wananchi (Ukawa) likijitokeza juzi na jana kuelezea kutoridhishwa kwao na hotuba hiyo kiasi cha wengine kujuta kushiriki katika maridhiano, kundi jipya la Tanzania Kwanza limeanzishwa.TANZANIA KWANZAUmoja wa Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba wanaojiita ‘Tanzania Kwanza‘ wameeleza kusikitishwa na kauli za baadhi ya wajumbe wenzao zenye muelekeo wa kuhujumu mchakato wa kupata Katiba mpya ambazo wamekuwa wakizitoa baada ya Rais Jakaya Kikwete kumaliza hotuba yake ya uzinduzi wa Bunge hilo Maalum.
Umoja huo ambao unaundwa na wajumbe kutoka chama tawala-CCM unadai kuwa na wajumbe 400, umedai kuwa viongozi waliotoa kauli hizo walionekana awali wakishangilia hotuba ya Rais pale aliposema yale waliyokuwa wanakubaliana nayo, lakini sasa watishia vurugu na kususia baadhi ya mambo wasiokubaliana nayo.

MKUMBA
Akizungumza na waandishi wa habari jana kwa niaba ya Mwenyekiti wa Umoja huo, Said Mkumba, alisema wameshangazwa na wajumbe hao waliotoa kauli nzito na kuacha kuweka utaifa mbele kwa kushawishiana hoja kuliko kulazimisha kutunga Katiba itakayoimarisha Taifa.

Alisema kuwa wajumbe walionekana kukerwa na baadhi ya maneno yaliyotamkwa na Rais Jakaya Kiwete ya kuwa na ustahimilivu wa kidemokrasia, ustaarabu na hekima ya uongozi na utu uzima.

Mkumba alisema kuwa hotuba ya Rais Kikwete imeweka wazi faida na hasara za mifumo yote ya Muungano wa nchi kwa hoja ili Watanzania wawe na fursa pana zaidi ya kutafakari na mwisho kuamua, hivyo wanashangazwa na baadhi ya wajumbe wenzao kutoa matamko hayo.

Naye Dk. Emanuel Nchimbi ambaye ni Mjumbe wa Umoja huo, aliwataka Wajumbe wa Bunge Maalum wasivumilie wala kuendekeza vitendo vya vurugu za makusudi vitakavyozuia au kuruhusu watu wachache waliweka rehani Bunge kwa kutengeneza mtaji wa kisiasa. MBATIA AJUTA
Hali ilizidi kudhihirisha mgawanyiko mkubwa ndani Bunge hilo, Mjumbe wa Bunge hilo, James Mbatia, ambaye ni Mbunge wa Kuteuliwa na Rais, ameowaomba radhi Watanzania kwa kushiriki kikao cha Kamati ya Maridhiano, ambacho kiliridhia kuvunjwa kwa kanuni ya 7 (1) ya Bunge hilo.

Kanuni hiyo inataka Rais azindue Bunge Maalum kabla ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba haijawasilisha Rasimu ya Katiba.

Akizungumza na wandishi wa habari mjini Dodoma, Mbatia ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, alisema anajutia uamuzi wake wa kushiriki kwenye maridhiano hayo.

Mbatia ambaye pia ni mmoja wa Ukawa, alisema maridhiano hayo yamekuwa na athari kubwa kwa wananchi kwa kuwa hakutarajia kwamba Rais Kikwete angekwenda kulihutubia Bunge kama Mwenyekiti wa CCM.

No comments:

Post a Comment