Friday, February 27, 2015

WASANII WA TANZANIA WANAUZUNGUMZIA UCHAGUZI MKUU WA 2015


 ‘IZZO BUSINESS’
Mkali huyu wa Bongo Fleva kutoka Nyanda za Juu Kusini, mkoani Mbeya, naye amefungukia uchaguzi mkuu kwa kueleza kuwa anaamini uchaguzi wa mwaka huu utakuwa wa amani na utulivu.
“Kuhusu mambo mengine kama vurugu na machafuko, hivyo havina nafasi kabisa,” alisema.


MRISHO MPOTO ‘MJOMBA’
Mkali huyu wa kughani na tungo za Kiswahili, yeye amefunguka:
“Kwanza kabisa uchaguzi umegawanyika sehemu mbili, kuna viongozi ambao wanahitaji madaraka na kuna wengine wanahitaji kufanya biashara.
“Vilevile hata wapiga kura nao wapo wanaojiandaa kufanya biashara kwa kujua kwamba wakimpigia kura kiongozi fulani, watanufaika na kitu fulani, tofauti na zamani ambapo utii na nidhamu kwa viongozi na wapiga kura ulikuwa mkubwa.“Sasa hivi hata wasanii nao wanafanya biashara kwa kutazama mgombea gani ana fedha ndiyo wanaenda kumfanyia kampeni, kwa hali hii tutegemee kuwa uchaguzi utakuwa wa kibiashara na si kutafuta kiongozi bora kwa taifa.”

KHADIJA KOPA ‘MALKIA’
Malkia huyu wa mipasho, ambaye pia ana uelewa mkubwa kwenye mambo yanayohusu siasa alisema: “Kwa kweli mi naona mwaka huu utakuwa mzuri kwa upande wa wanawake kwa sababu katiba inayopendekezwa ikipitishwa kutakuwa na usawa katika kila nafasi ya uongozi kati ya wanaume na wanawake.
 
BABY MADAHA.
Mwanadada huyu anayefanya poa kwenye gemu la Bongo Fleva, alifunguka: “Naamini kuwa katika uchaguzi wa mwaka huu bado nafasi ya wanawake kwenye urais itakuwa ni ndogo lakini kwa upande wa nafasi za ubunge na udiwani wanaweza kufanya vizuri zaidi na watu wakashangaa kuona viti vingi vikichukuliwa na wanawake wenye kiu ya kuleta maendeleo ndani ya taifa letu. Mi naamini wanawake tunaweza.” EMMA-NUEL SIMWINGA

KULWA KIKUMBA ‘DUDE’
Msanii huyu wa filamu alisema “Mtazamo wangu kwa kweli mi naona uchanguzi wa mwaka huu utakuwa mgumu kuliko changuzi zote zilizowahi kutokea ndani ya taifa hili, kwa sababu watu wengi wameamka na wanajua nini wanafanya.
“Lakini pia wananchi wanaanza kuwakataa baadhi ya vigogo wanaokuja mtaani kwa mbwembwe na baada ya kupata kile wanachokitaka wanakimbia na kujali maslahi yao binafsi, kwa hali hii baadhi ya vigogo wataanguka sana kwenye nafasi zao, tumeona kwenye Serikali za Mitaa mambo yalivyokuwa, tusubiri lakini uchanguzi utakuwa mgumu sana, vijana wengi walikuwa hawapigi kura lakini sasa wamejua maana halisi ya kura zao”.
AMINI MWINYIMKUU
Msanii huyu wa muziki wa Bongo Fleva naye alifunguka: “Uchaguzi wa mwaka huu mimi naona utakuwa mzuri kwa sababu kila chama kina mashabiki na wapenzi wake na kikubwa ambacho kinaonekana ni kwamba wananchi wengi wameelewa nini maana ya kupiga kura kwa lengo la kupata viongozi ambao wataleta maendeleo ndani ya taifa letu.”

 

EMMANUEL ELIBARIKI ‘NAY WA MITEGO’
Msanii huyu wa Bongo Fleva ameeleza mtazamo wake kuelekea uchaguzi mkuu:
“Uchaguzi wa mwaka huu unaweza kuwa mgumu sana kwa sababu watu wameelimika tofauti na zamani ambapo watu walikuwa wanafanya mambo bila kujielewa. Vijana na watu wengine wameelimika na kujua kiongozi gani anafaa na nani hafai.“Ule ujanja wa kusema baadhi ya vyama vitaiba kura nadhani hilo litakuwa gumu sana mwaka huu kwani kila mtu anapiga kura akiwa anajua haki zake za msingi.”
 ‘IZZO BUSINESS’
Mkali huyu wa Bongo Fleva kutoka Nyanda za Juu Kusini, mkoani Mbeya, naye amefungukia uchaguzi mkuu kwa kueleza kuwa anaamini uchaguzi wa mwaka huu utakuwa wa amani na utulivu.
“Kuhusu mambo mengine kama vurugu na machafuko, hivyo havina nafasi kabisa,” alisema.

No comments:

Post a Comment