Monday, February 24, 2014

MH;SAMWELI SITA: NITAGOMBEA UENYEKITI KWENYE BUNGE MAALUMU LA KATIBA KWANI NINA SIFA.






Waziri Samweli Sita.
Hii ni mara ya kwanza kwa Sitta ambaye alikuwa Spika wa Bunge la Tisa kuweka wazi uamuzi wake huo. Mwingine anayetajwa ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali wa zamani na Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM), Andrew Chenge.
Dodoma.
Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta amesema atagombea uenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba kwa sababu anaamini kuwa ana sifa za kutosha.
Hii ni mara ya kwanza kwa Sitta ambaye alikuwa Spika wa Bunge la Tisa kuweka wazi uamuzi wake huo. Mwingine anayetajwa ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali wa zamani na Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM), Andrew Chenge.
Sifa za mtu anayepaswa kuongoza Bunge hilo ni kuwa na shahada ya sheria kutoka katika chuo kinachotambulika pia kuwa na uzoefu wa kuendesha mijadala kama ya Bunge.
Akizungumza na gazeti hili jana, Sitta alisema pamoja na propaganda chafu zinazoenezwa dhidi yake, hatakata tamaa na kwamba ataendelea na msimamo wake huo ili nchi ipate Katiba bora.
“Sheria ya Mabadiliko ya Katiba imeainisha sifa za mtu anayetakiwa kuwa mwenyekiti na mimi nina sifa na nina mipango mizuri ya kuwafanya Watanzania wapate Katiba bora kama ndoto ya Rais wetu (Jakaya Kikwete) ilivyo,” alisema.
Alipoulizwa kuhusu njama za kumzuia asigombee nafasi hiyo, Sitta alisema “Haishangazi watu hao kutumia mbinu chafu… Hawana maadili, ndiyo maana wananihofia lakini sishtuki hata kidogo.”
Sitta ambaye pia ni mbunge wa Urambo Mashariki (CCM), alisema wabaya wake wamekuwa wakieneza maneno ya uongo kwamba ikiwa atakalia kiti hicho, atasimamia mpango wa Serikali tatu.
“Wanasema Sitta ataruhusu Serikali tatu, sasa nashangaa maana wajumbe ndiyo wenye mamlaka hayo… wanaeneza propaganda kuwa nina mkataba na wapinzani ndiyo maana wananiunga mkono. Wanasema mambo ya ovyo kabisa,” alisema.
Sitta alisema wapinzani kama walivyo wajumbe wengine kutoka CCM na makundi mengine, wanamuunga mkono kwa kuwa wanaamini akikalia kiti hicho ataendesha Bunge hilo kwa misingi ya uwazi na haki.
“Mimi sina mkataba na wapinzani ila wao kama watu wengine wananiunga mkono kwa sababu wanajua nitatenda haki, nina rekodi nzuri katika kuliendesha Bunge la Tisa wala hiyo haina mashaka,” alisisitiza Sitta.
Sitta na Chenge
Kumekuwa na msuguano na kampeni za chini chini kati ya kundi la Sitta na Chenge, lakini habari zilizopatikana jana kabla ya Sitta kutangaza kuwania nafasi hiyo, zilisema CCM walikuwa wakikusudia kuwaondoa makada hao, na kumpendekeza Mathias Chikawe badala yao.
Ilielezwa kuwa hatua hiyo imefikiwa kutokana na mpasuko mkubwa ndani ya chama hicho unaotokana na wapambe wa makada hao kuanza kupakana matope.
Hata hivyo Chikawe alisema hana taarifa yoyote kuhusu mpango huo. “Ahaaa! Sina taarifa hiyo, sijawahi kufikiria kushika nafasi hiyo, wewe (mwandishi) ndiyo unaniambia na nimeshtuka sana, lakini nitafuatilia,” alisema Chikawe.
Kwa upande wake, Chenge juzi alisema hana sababu ya kulumbana na watu aliowaita kuwa hawataki kuelewa na kwamba tayari CCM kilikuwa kimetoa mwelekeo wake.
Hata hivyo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema chama hicho hakijatoa msimamo wa mtu kinayetaka agombee nafasi hiyo kwani hakuna kikao chochote kilichojadili suala hilo.
“Kama uamuzi unafanywa, lazima vikao vya chama vikae, lakini hadi sasa kwa uelewa wangu hakuna kikao chochote cha chama ambacho kimeketi na kuamua suala hilo,” alisema Nnauye.

Kauli ya Nnauye iliungwa mkono na ile ya Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, William Lukuvi ambaye alisema chama hakijatoa mwongozo wowote kuhusu suala hilo kwa kuwa muda wake bado.
“Chama hakijatoa mwongozo wowote ingawa tunajua watu wameanza kuumana kwa hilo, wako kama saba,” alisema Lukuvi.
Lukuvi ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), alikuwa akijibu tuhuma zilizotolewa dhidi yake kwamba ndiye anayeshawishi Sitta asiwe mmoja wa wagombea katika kinyang’anyiro hicho ili kulinda mwonekano wa Spika wa Bunge, Anna Makinda.
“Wanahofia endapo Sitta atafanikiwa kupata uenyekiti na kuendesha vizuri Bunge na Makinda akaja kuendesha Bunge la Bajeti ataonekana kupwaya sana,” kilisema chanzo chetu.
Lukuvi alikanusha kuhusika na mpango huo akisema: “Mimi nahusika vipi kwenye hilo. Kwanza kama chama hatujatoa mwongozo lakini hatuwezi kutoa mwongozo kabla Bunge halijatoa kanuni za namna ya kumpata mwenyekiti.”
Lukuvi alikiri kufahamu kuwapo kwa vita ya uenyekiti, lakini akasema yeye haoni mantiki ya kuhusishwa kwake. “Mimi najua watu wameshaanza kuumana lakini kwa nini sasa, wakati hata kanuni hazijatoka na chama hakijatoa mwongozo,” alihoji.

No comments:

Post a Comment